Makamu wa Rais wa Serikali ya Jamuhuri ya Muungano waTanzania Dkt. Philip Isdori Mpango Amesema baada ya miaka 60 ya Muungano, Tanzania inajivunia maendeleo katika sekta mbali mbali ikiwemo Sekta ya Elimu ambayo inatolewa bila ubaguzi kwa wote.

Dkt. Mpango ameyasema hayo mara baada ya kufungua Skuli ya Sekondari ya Maziwang’ombe ikiwa ni Muendelezo wa shamrashamra za maadhimisho ya miaka 60 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.

Amesema kuimarishwa kwa miundombinu ni jitihada za makusudi zinazofanya na serikali zote mbili ili Kuandaa mazingira mazuri ya upatikanaji wa huduma hiyo.

Akifafanua Zaidi Dkt. Mpango amesema miongoni mwa matunda ya Muungano ni uwepo wa Vyuo Vikuu visivyopungua 7 ambapo kabla ya Muungano Zainzibar Matunda hayo hayakuwepo. 

Amewataka wazazi kuungamkono jitihada hizo kwa kusimamia vyema maendeleo ya Elimu ya watoto wao sambamba na kutoa kipaombele katika kuwapatia Elimu watoto wa kike.

Wakati huo huo Dkt. Mpango amewataka wananchi kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi kwa kupanda miti ya matunda pamoja na ya kivuli.

Nae Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Mhe. Ali Abdulghulam Hussein amesema ufunguzi wa Skuli ya ghorofa 3 ni kitendo cha kihistoria kwavile haikuwahi kufunguliwa Skuli yenye hadhi kama hiyo hapa Zanzibar.

Amempongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Hussein Ali Mwinyi kwa kazi kubwa anayoifanya katika kuwaletea Maendeleo Wananchi.

Kwa upande wake Katibu Mkuu Wizara ya Elimu Ndu. Khamis Abdullah Said amesema Ujenzi wa Skuli ya Sekondari ya Maziwang’ombe ulianza mwenzi mei mwaka 2023 ambapo umegharimu jumla ya shilingi bilioni 6.2 hadi kukamilika kwake.

Aidha amesema Wizara imeweka vifaa vya maabara ambapo mfumo wa gesi anuwai Umeunganishwa ili kuwezesha matumizi bora ya maktaba hiyo.